‘’Ukijishusha thamani  na  ulimwengu  utakushusha  thamani”.

– Ophra Winney

Kujikubali ulivyo ni kujiponya. Bila wewe mwenyewe kujikubali, hakuna atayekukubali ama kukubali unachokifanya. Mwenyezi  Mungu  anakupenda  sana.  Alikuumba  kwa sura na mfano wake. Hakukuumba kwa bahati mbaya. Usijikatae.  Usijidharau. Usijione kama mtu wa bahati  mbaya.  Hakuna  mtu  anayeweza kuwa  kama wewe hapa duniani. Wewe ni  wa  tofouti. Una kitu  ambacho  watu wengine  hawana. Wewe ni wewe. Miongoni mwa watu ambao dunia inasubiri kuona mafanikio yao ni ‘Wewe’. Dunia  inasubiri  kuongozwa na mawazo yako. Kuna watu wanasubiri  kuajiriwa na kampuni yako. Ukikata tamaa  utakuwa  umeua  ndoto za watu wengi sana. Amini kila unalotaka kupata utalipata hata kama ni kwa kuchelewa. Wewe ni mshindi sio mshindwa.

Mwanamitindo Ophra Winney anasema, ‘’Ukijishusha thamani  na ulimwengu  utakushusha thamani”. Tafadhari  nakuomba usijishushe thamani. Jithamini. Wewe ni wa thamani sana katika dunia hii. Wewe ni wewe, hakuna anayeweza kuliziba pengo lako. Mwaka 2012 gazeti la Kiongozi linalomilikiwa na Kanisa Katoliki  nchini Tanzania lilichapisha makala yangu iliyokuwa inasema: ‘’Krismas bila Kristu sio Krismas”.  Msomaji mmoja alinitumia ujumbe mfupi kupitia simu yangu ya kiganjani. Ujumbe wake  ulisomeka:

Ndugu  yangu  William  Bhoke,  hii   ni  Krismas yangu ya 50, kwa maana hiyo nina miaka 50. Ninachosikitika ni kwamba  sina  hata mtoto wa kusingiziwa, sina uwanja wala nyumba. Niliajiriwa miaka 12 iliyopita ninaelekea  kustaafu kazi lakini maisha yangu hayana nyuma wala mbele. Nimekata tamaa kabisa. Nimejikataa na kukataliwa. Siamini kama nitafanikiwa tena. Ninaomba unipe muongozo mpya wa maisha.

Mwandishi wa vitabu, Mark  Kay Ash anasema, “Mungu hakuwa  na  muda  wa  kuumba mtu ambaye hana maana, bali mtu wa maana tu’’. Wewe ni mtu wa  maana sana. Una sababu za kuzaliwa.  Kataa  kujikataa.  Kujikataa  ni kuhisi  kuwa  wewe si mtu muhimu. Ukweli ni kwamba, wewe ni  mtu mhimu sana  katika sayari hii ya dunia. Mwenyezi  Mungu hakukuumba  kwa  bahati mbaya.  Kwa  Mungu  hakuna  bahati  mbaya. Kwa Mungu hakuna bahati na-sibu. Kwa Mungu kila kitu  ni uhakika.  Mfalme Daudi alimtukuza Mungu kwa maneno haya:

“Ninakusifu (Mungu) kwa kuwa nimeumbwa kwa namna ya ajabu ya kutisha’’  (Zab139:14).

Usimwaibishe Mungu  kwa  kuishi  maisha ya kujikataa. Kujikataa ni kumwaibisha  Mungu aliyekuumba kwa sura na mfano wake [Rejea Mwanzo 1:26-27]. Kujikataa ni kumwambia Mungu: ‘Hukuniumba vizuri’. Kujikataa ni kuzikataa  baraka za Mungu katika maisha yako. Kuanzia leo kataa kujikataa. Kataa kuwa maskini. Kataa kuwa ombaomba. Kataa kuwa mlevi. Kataa kuwa mzinzi. Kataa  kuwa  mchepuko.  Kataa  kuwa  muongo. Kataa kuwa mnafiki. Kataa  kuwa  na  kiburi.  Kataa  kuwa  na majivuno.  Kataa  kuwa  na  hasira. Kataa  kuwa  mfano  mbaya  katika  jamii. Usijikatae.  Wewe  ni  mtoto   wa  Mungu.

 

Kujikataa ni kukubali kushindwa kufanikiwa. Unapojidharau unakuwa adui wa mafanikio yako.  Iko hivi:  Kutokuwa  na  mipango  mikubwa  katika  maisha yako ni  kujikataa. Kutokujistahi ni kujikataa.  Kutojipenda ni kujikataa. Kutokujiamini ni kujikataa. Kutokujitakia  mema  ni  kujikataa. Kuishi na chuki moyoni mwako ni kujikataa. Kutokusamehe ni kujikataa.  Kuwawazia  watu  wengine  mabaya ni kujikataa. Leo andika upya historia maisha yako. Kuanzia leo jiwekee agano la kufanikiwa. Jikubali  kuanzia leo na  siku zote zijazo.  Jipende  kuanzia leo  na siku zote  zijazo.  Jiamini kuanzia leo na siku zote zijazo. Jisamehe kuanzia leo na  siku zote zijazo. Jiheshimu kuanzia  leo na siku zote zijazo.

Mwanasaikolojia wa Uswisi, Carl  Jung  anasema, ‘’Kujua giza lako mwenyewe ni  mbinu  bora  ya  kukabiliana  na giza la watu wengine’’. Kila mtu ni kiongozi wa maisha yake na maisha ya wengine. Usipojiongoza wewe mwenyewe, huwezi kuwaongoza wengine. Kesho inakuja. Usipojiandaa vizuri leo, kesho yako  itakuwa na lawama. Fanya kazi kwa bidii ili kesho yako iwe njema. Lawama  ni  mtaji wa walioshindwa kufanikiwa. Acha kulalamika. Jiondoe kwenye  kundi  la  watu wanaolalamika  kwa  kila  jambo. Waandishi wa kitabu cha The Power of No, James Altucher na Claudia Altucher wanasema, ‘’Kulalamika ni  kukimbiza  fursa. Unapoacha kulalamika unaanza kuona kila hali ya fursa. Unafungua mlango wa kupata mawazo mapya’’. Hakuna aliyefanikiwa kwa kulalamika. Usilalamike.

Mwandishi T. L. Osbon  anasema, “Ukiacha kujifunza unaanza kufa’’. Tafuta wazo jipya kila siku. Kumbuka: Usipotumia nguvu nyingi kuwaza mawazo  yatakayoibadili dunia, ni lazima utaajiriwa na watu waliotumia nguvu nyingi  kuwaza mawazo yaliyoibadili dunia. Mwandishi wa vitabu vya  Kiroho, Tony  Evans anasema, “Watu wengi wanatumia muda wao mwingi kuishi maisha ya watu wengine’’.  Acha  kupoteza  muda  wako wa  thamani  kwa  kuiga  kuishi  maiha  ya mtu  fulani. Ishi  maisha  yako.

Tembea kwenye kusudi  la  Mungu. Mungu  ana mpango na wewe. Anataka jambo  kubwa  litokee  kupitia  wewe.  Anataka  atukuzwe  kupitia  wewe. Wewe ni  mpakwa  mafuta  wa  Bwana.  Una  upako  wa  ajabu. Uwepo  wako  duniani sio  ajali  ya  kibaiolojia, bila  kujali  mazingira  yaliyozunguka  kuzaliwa  kwako. Uko hai kwa sababu ya Umwilishwaji wa Ki-Mungu uliopitia kwa wazazi wako. Kutungwa  kwako  mimba  na  kuzaliwa  kwako ni uthibitisho kwamba, Mungu ana mpango na wewe. Usijutie  kuwa miongoni  mwa  wanafamilia wa kibinadamu wanaoishi katika sayari hii ya dunia. Jambo moja na la mhimu ambalo kila mtu anapaswa kulifahamu ni kwamba; Mungu hawezi kuruhusu chochote kije katika maisha yako ambacho hutaweza kukabiliana nacho. Kumbuka: Pale unaposema, hapa  nimefika mwisho, Mungu anasema,  ‘Huu ni mwanzo mpya’.  Mtume Paulo ameandika hivi:

 

‘’Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya mwanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili’’ [1Wakorintho 10:13]

 

Kumwamini Mwenyezi  Mungu  wakati  wa  raha ni rahisi mno kuliko kumwamini  wakati wa shida, na utahitaji imani kuendelea kumwamini wakati wa dhiki. Vipindi vigumu katika maisha yetu hutokea kwa kila mmoja wetu. Kuamini  ya  kwamba Mungu ana makusudi ya lazima kukuondolea vikwazo katika maisha  yako ni vigumu sana wakati mwingine, lakini imani ndicho kitu cha muhimu  zaidi unachotakiwa kuwa nacho katika kipindi hiki ambacho dunia imekata tamaa. Amani ya Mungu, ambayo huzidi hekima na maarifa yote ya kibinadamu, ni kuliamini neno la Mungu kwamba ni la kweli. Bila imani hutaweza kumfurahisha Mungu. Imani ni ufunguo wa nguvu, uwezo na neema ambavyo Mungu ametupangia. Kwa ufupi, Mungu ni mkubwa kuliko wewe na matatizo yako. Jikubali.

KOSA  KUBWA NI   KURUDIA  KOSA

’Kama  hufanyi makosa, hufanyi  chochote  katika  maisha’’.

                                                                                   – John  Wooden

Kosa ni  alama ya  uhai.  Kama hauko hai  huwezi  kutenda  kosa.  Mwanamichezo  wa Marekani  John  Wooden  anasema, ‘’Kama hufanyi makosa, hufanyi  chochote  katika maisha’’. Huwezi kuishi kwa muda mrefu bila  kutenda  kosa.  Mwanadamu ni tajiri wa makosa. Tunajikuta kila mara katika  makosa  na  dhambi. Tunamkosea Mungu na wenzetu. Tena, kuna wakati tunamkosea Mungu  na wenzetu kwa bahati mbaya au kwa kukusudia. Katika sura  hii  nitakufundisha umhimu wa kukiri kosa pale unapokuwa umetenda kosa.  Nitakufundisha pia namna ya kulitazama kosa kama fursa ya kujifunza jambo jipya. Katika roho ya ukimya na tafakuri  mwanana, ninakualika usafiri pamoja nami katika makala hii inayolenga kuyaangazia maisha yetu.

Kosa kubwa ni  kudhamiria  kutenda  kosa.  Kosa  la  kimakusudi  ni  kosa  kubwa.  Ni kosa ambalo linakugharimu. Usikusudie kutenda kosa kwa lengo la kumkomoa mtu ama kumshushia heshima yake na utu wake, kinyume chake utakuwa wewe ndiye mhanga wa kosa ulilokusudia mwenyewe kulitenda.

Jifunze jambo  jipya  kila unapokuwa  umetenda  kosa.  Katika safari ya mafanikio, kosa ni fursa ya kujifunza mbinu mpya  ya  kufanikiwa.  Huwezi  kufanikiwa  kwa kuyaficha  makosa yako. Huwezi kuwa mtu mwema kwa kuyaficha makosa yako. Neno la Mungu linasema, ‘’Afichaye makosa yake hatafanikiwa; lakini anayeyaungama na kuyaacha atapata rehema’’ [Mith 28:13].

Kila kosa lina jambo la kujifunza ndani yake. Unapotenda  kosa, jiulize kwa nini  umetenda  kosa.  Je, umetenda kosa kwa kudhamiria au ni kwa bahati mbaya? Je, umejifunza nini kutokana na kosa ulilolitenda? Je, utarudia kulitenda kosa hilohilo? Kiri kosa lako halafu omba msamaha kwa kosa ulilolitenda. Upotendewa kosa, jiulize kwa nini umetendewa kosa. Huwezi kutendewa kosa pasipo sababu. Sababu ya kutendewa kosa inaweza kuwa ya kukusudi na inaweza pia isiwe ya kukusudia. Jiulize; Je, hili kosa nililotendewa nimetendewa  kwa  bahati  mbaya  au ni kwa makusudi maalumu? Je, aliyenitendea  kosa  alikuwa  katika  hali gani na katika mazingira gani? Je, kuna faida yoyote  ambayo  nitaipata  endapo  nitamchukia huyu aliyenitendea hili kosa? Msamehe kwa moyo wa dhati aliyekukosea.  Kosa ni ujumbe kuwa unafanya au umefanyiwa kitu fulani.

Mtoa hotuba wa Marekani, Roger Von Oech alipata kuandika hivi, ‘’Ukifanya kosa, litumie kama njia ya kuvukia kwenda kwenye wazo jipya ambalo usingeligundua  kama  pasingekuwepo  na  kosa’’. Yawezekana  historia ya maisha  yako  inakukatisha tamaa. Usikate tamaa. Nisikilize kwa umakini hapa. Tunaweza kujifunza  mbinu bora za kutoshindwa tena kutokana na makosa yetu ya awali  na  kufanya vizuri pale tuliposhindwa. Jambo hilo linawezekana.

Hatuwezi kufanya vizuri pale tuliposhindwa  awali ikiwa tunapendelea kuhalalisha  makosa yetu. Tunapokiri makosa yetu na kuomba msamaha, tunajenga mazingira ya amani ndani ya mawazo yetu. Hebu akili zetu zipewe nafasi na kazi ya  kutafakari mema, ndipo mioyo yetu itajazwa amani. Sifa kubwa ya maskini wa kiroho na kiuchumi ni lawama. Unapotenda kosa, usitangulize lawama. Weka lawama pembeni. Kiri kwanza kosa lako. Kosa halitatuliwi kwa  kulalamika.  Kosa halitatuliwi kwa kujilaumu au kwa kuwalaumu wengine.

Maisha ni mfano. Maisha ya watu wengine ni mfano kwako. Maisha yako ni mfano kwa  watu  wengine.  Mwandishi  Gilbert  West anasema, ‘’Mfano ni kitabu  ambacho  watu  wote  wanaweza  kusoma’’. Jifunze  kutokana na makosa ya watu wengine. Mtu mwenye busara makosa ya wengine, kwake ni shule. Anajifunza somo fulani.  Kosa kubwa  ni kuyafurahia makosa ya wengine. Makosa ya wengine yasigeuke kuwa furaha kwako bali yageuke kuwa funzo kwako.

Jifunze kuwa mkweli na kuupenda ukweli katika maisha yako.  Mwalimu  Nyerere  alisema, ‘’Ukweli  ni  ukweli  hata  kama  hakuna  mtu  anayesema  ukweli.  Uongo  ni  uongo  hata  kama  watu  wote  watasema  uongo’’.  Uongo  unaponya  kwa  muda  mfupi  lakini  unaumiza  kwa  muda  mrefu.  Unapotenda  kosa  la  aina  yoyote,  kubali  ukweli  uweke  bayana  uhalisia  la  kosa  ulilolitenda. Kubali  ukweli uwe mwalimu wa maisha yako.  Kubali  ukweli  ukupe  amani  ya  moyoni. Mwandishi wa vitabu wa Uingereza George Orwell alipata kuandika; ‘’Katika dunia yetu hii iliyojaa ulaghai, utapeli na udanganyifu tendo la kusema ukweli  linachukuliwa  kama la kimapinduzi, lakini  ukweli ndio unaotakiwa’’.

Uongo  unapotea, lakini  ukweli  unaishi  milele.  Mwanaharakati  Clarence  W. Hail alipata kusema, “Unaweza  kuuweka  ukweli  kaburini  lakini ukweli  hauwezi kukaa kaburini”. Wayahudi walipomuua Yesu Kristo walimweka kaburini. Walifikiri wameuzika ukweli. Walifikiri wamemaliza kazi, lakini  ukweli ni kwamba Yesu Kristo hakukaa kaburini. Alifufuka. Ukweli wa Yesu Kristo kufufuka ulishinda. Unapotenda  kosa,  usiliweke  kaburini.  Ukilificha  kosa  lako  kaburini, ukweli utalifichua. Methali ya Kifaransa inasema, “Watu binafsi  watakufa lakini  ukweli  ni wa milele”. Ismail Haniyeh alipata  kusema, ‘’Baadhi   ya watu  hudhani kuwa ukweli  unaweza kufichwa kwa kuuzuia  kidogo  au kuupamba lakini kadiri muda unavyozidi kwenda kilicho cha kweli  hudhihirishwaa  na uongo  kutoweka’’. Kukiri kosa ni kujiponya kiroho na kimwili.