Rais wa Tanzania, John Magufuli amesema Serikali haitafunga mipaka wala kuwazuia watu kutoka ndani ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona kwa sababu kufanya hivyo kutasababisha madhara ndani na nje ya Tanzania.
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo Ijumaa Aprili 10, 2020 katika Kanisa Katoliki Parokia ya Mlimani Wilaya ya Chato mkoani Geita alipoungana na waumini kusali ibada ya Ijumaa Kuu iliyoongozwa na Padri Innocent Sanga wa jimbo Kuu Katoliki la Mbeya.
Taarifa iliyotolewa na mkurugenzi wa mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa inamnukuu kiongozi mkuu huyo wa nchi akisema Serikali ya Tanzania imeamua kutowazuia watu ndani ya nyumba zao wala kufunga mipaka kwa kutambua madhara makubwa yanayoweza kujitokeza kutokana na kufanya hivyo ndani ya nchi na kwa nchi nane ambazo zinategemea kupata huduma na bidhaa kupitia Tanzania hususani Bandari ya Dar es Salaam.